I WISH U A MARRY XMASS & HAPPY NEW YEAR 2012

click the word video above 2 watch the clips & cloz 2 back

Saturday, November 20

Mapenzi ni afya, ni kila kitu lakini yana kanuni zake!


Haihitaji papara kuamua kuhusu mwenzi wa maisha yako. Kuna fahari ya macho na kinachogusa mtima. Usimuone barabarani ni mzuri, ukakurupuka. Unatakiwa ujadiliane na moyo wako halafu mpate jibu linalokubalika. Kupata mwenzi wa maisha ni sawa na Serikali ya Umoja wa Kitaifa. Tofauti na ile ya Zanzibar au Kenya, hii inahusisha maridhiano kati ya macho na moyo. Macho yanaona na kuvutiwa, moyo unaguswa. Kwa mantiki hiyo, ni kosa kujiaminisha kwamba unapenda ikiwa moyo wako haujakubali. Lakini haiwezekani moyo ukapenda ikiwa macho yamekataa. Macho yanaona, ubongo unatafsiri halafu moyo unapokea. Umemkubali kwa jinsi alivyo, hapo ni sawa. Lakini unatakiwa kujiuliza maswali mengine 50 kuhusu yeye, halafu upate majibu ambayo yanaridhiwa na kila upande. Usifanye chaguo ambalo litaufanya moyo wako usinyae. ONYO: Kamwe usiruhusu moyo wako usinyae kwa sababu hiyo ni sawa na ugonjwa hatari. Moyo unaposhindwa kufanya kazi yake barabara, hutema sumu ndani kwa ndani ambayo inaweza kukusababishia matatizo makubwa nap engine kukua haraka. Kuwa makini. Maswali ya kujiuliza ni haya; KABISA NIMEMRIDHIA? Hapa kuna maana kuwa tayari umemkubali lakini jiulize tena na tena kuhusu yeye. Kama kuna shaka ndani yake usilazimishe, badala yake pitisha uamuzi mmoja pale ambapo umeona majibu yanakuja chanya kila ulipojiuliza. NIPO TAYARI? Binadamu hajakamilika, pengine kuna mambo yanayomzunguka mwenzi wako. Watu wa pembeni wanazungumza, lakini pia si ajabu ikawa kuna vikwazo vya kifamilia. Swali hili linachukua nafasi katika eneo hilo. Jiulize kama upo tayari kukabiliana na presha za watu na ndugu ilimradi uhakikishe unambakiza kwenye himaya yako. Isitokee ukasema upo tayari leo lakini baada ya muda ukamfanya mwenzako ajute. Jiridhishe leo kwa faida ya maisha yenu kwa jumla. U-tayari wako uwe na maana kuwa hata miaka 10 ijayo, utamtetea popote kwamba ulilolisimamia leo, utaendelea nalo kila siku mpaka Mungu atakapoamua kutumia mamlaka yake kuwatenganisha. SITAMCHOKA? Usithubutu kupenda kwa fahari ya jicho la leo. Nimekutaka ujadiliane na moyo wako kwa sababu kuna vitu vingi vya kujiridhisha kabla ya kuamua kuzama moja kwa moja. Ikiwa kuna dalili kwamba ipo siku utamchoka usithubutu kumpotezea muda. Mwenzi wa maisha ina maana ni mtu wa furaha yako kwa maisha yako yote. Kwamba yeye atakuwa sehemu ya maisha yako. Hivyo, huyo hatakiwi kuchokwa bali anastahili hifadhi ya kudumu moyoni kuliko mwingine. Mtu ambaye unaweza kumchoka mbele ya safari utamjua tu kwa kujiuliza. Ikiwa kuna penzi la kweli, hakika utaona ni kiasi gani linavyomea. Hutakuwa na shaka ya aina yoyote juu yake na utakubali kwamba furaha anayokupa leo, haitabadilika. Kuna penzi la usanii, kama hilo ndilo linalokuongoza basi ni vema ujitenge. Nina maana kuwa endapo humpendi kutoka moyoni ila unamdanganya, jitenge haraka kwa sababu mbele utamchoka, utamsumbua na utamsaliti. VIPI MAUDHI YAKE? Mpenzi wako ni binadamu siyo malaika. Hivyo ndivyo na wewe ulivyo. Nyoye ni viumbe dhaifu, kwahiyo kila mmoja ana upungufu wake lakini kwako ni vizuri ukajiuliza endapo maudhi yake unaweza kuyavumilia. Ni kosa kubwa kufukia mashimo kwa yale yanayokukwaza kwa mwenzi wako. Amua leo, ikiwa unaona kila kitu kinawezeka, kwamba pamoja na kasoro zake lakini anavumilika na upo tayari kufanya naye maisha, basi nenda mbele zaidi. Ruhusu moyo wako uamue katika maudhi yanayokusumbua kutoka kwa mwenzi wako. Moyo wako upime kwamba ubora wake upo juu kuliko kasoro zinazokutibua. Hapo unangoja nini tena? Mng’ang’anie huyo huyo, ukitaka asiye na kasoro utasubiri sana. NAWEZA KUONGOZANA NAYE? Hili siyo swali la kudharau hata kidogo. Kuna watu wengi wapo kwenye ndoa lakini hata siku moja huwezi kuona wameongozana na wenzi wao. Kuna vitu vingi vinawasibu, angalia nawe yasije yakakukuta kwenye safari yako. Akuridhishe kwa muonekano wake, kwahiyo uwe na imani kuwa hata ukiongozana naye barabarani utakuwa ni mwenye kujiamini. Hapa kuna la kujifunza zaidi. Hakuna maana kuwa utashindwa kuongozana naye kwa sababu ni mbaya, la hasha! Inawezekana mwenzi wako ni mzuri sana, kwahiyo mkiongozana watu huwashangaa. Pia, mwenzi wako anaweza kuwa na umbo kubwa, mnene, hivyo macho ya watu barabarani yanaweza kukufanya ukajiona mnyonge.