I WISH U A MARRY XMASS & HAPPY NEW YEAR 2012

click the word video above 2 watch the clips & cloz 2 back

Thursday, August 5

TAHADHARI NONDOOOZ ZA CHUMA KIMOJA.

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania
Tahadhari Kuhusu Ongezeko la
Vyuo Vikuu Batili (Degree Mills)

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imepewa mamlaka ya kisheria kuthibiti na kusimamia ubora wa viwango vya elimu na mifumo inayotumiwa na vyuo vikuu katika kukidhi viwango vya ubora wa elimu ya juu, kusimamia uthibiti na kuhakiki uhalali na viwango vya kitaaluma vya tuzo za digrii na stashahada zinazotolewa na taasisi za elimu ya juu ndani na nje ya nchi.

Ifahamike kwamba, tuzo hizo zinahusisha pia digrii za heshima ambazo vyuo vikuu vimepewa mamlaka ya kuwatunuku watu ambao chuo husika kimeona ama mtarajiwa kupewa digrii hiyo ametoa mchango mkubwa wa kitaalam katika eneo lake la kitaaluma, au ametoa mchango mkubwa katika masuala ya kuhudumia ustawi wa jamii. Utoaji wa tuzo za aina hii kwa kawaida ni uamuzi wa vyuo husika kwa kutumia mifumo yao iliyowekwa kisheria inayotoa mamlaka kwa chuo kufanya hivyo.

Kwa mantiki hiyo, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inatambua na kukubali uhalali wa digrii za heshima zilizotolewa na vyuo vikuu vilivyothibitishwa na vinavyotambuliwa na serikali au taasisi zilizokasimishwa mamlaka ya kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria. Hata hivyo, digrii za heshima haziwezi kutumika kama sifa ya kitaaluma, kwenye jina la mhusika au vinginevyo, katika kutafuta ajira, kupandishwa cheo, au kama msingi wa kujiendeleza kielimu.

Katika miaka ya hivi karibuni Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania imebaini ongezeko la tuzo za digrii za uzamivu za heshima, yaani “honorary doctorates (honaris causa)” zikitolewa kwa watu wenye haiba na wadhifa mkubwa katika maeneo mengi ya Afrika. Hali hii pia inaongezeka kujitokeza kwa kasi nchini Tanzania. Haishangazi kuona kwamba katika kipindi cha muongo mmoja uliopita na hadi sasa hivi, watu maarufu wamekuwa wakitunukiwa digrii za aina hii kutoka katika taasisi ambazo kutambuliwa kwake kunatia shaka siyo nchini Tanzania tu, bali hata katika nchi zilimo taasisi hizo.

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inastushwa sana na suala hili la ongezeko na nyendo za taasisi na vyuo vikuu visivyotambuliwa nchini Tanzania na kwingineko duniani, ambavyo vimepewa jina la utani “viwanda vya kutengeneza digrii au stashahada”, yaani “degree mills”, ambavyo vinawadanganya Watanzania kwa kuwatunuku digrii za uzamivu za heshima.
Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inatambua madhumuni potofu ya ongezeko la vyuo hivyo bandia hapa nchini kwetu. Mantiki na matokeo ya digrii zitolewazo na vyuo hivyo batili kwa wanaotunukiwa na kwa jamii wanayoitumikia ni hatari na inawapunguzia heshima watunukiwa hao wao wenyewe na taifa zima kwa ujumla.

Kwa hiyo basi, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inatahadhalisha umma kuwa makini ili kuepuka wasitapeliwe na taasisi ambazo ni “viwanda vya kutengeneza digrii”, ambazo kwa hakika nia yao ni kujipatia pesa au kutafuta umaarufu kwa njia zisizo halali. Licha ya kutunuku digrii bandia za heshima, taasisi hizi pia zimewatapeli watu wengi pamoja na watanzania kwa kuwatunuku digrii, digrii za uzamili na hata za uzamivu (yaani doctorate degrees) bila ya wahusika kufanya kazi yoyote ya kitaaluma inayolingana na matakwa ya kutunukiwa digrii walizopewa, kwa kuwa tu waliweza kulipia gharama za digrii hizo.

Baadhi ya taasisi zinazotoa tuzo za digrii, na digrii za uzamivu za heshima zimefika mbali zaidi kwa kudai kuwa eti wanafanya hivyo kwa ajili ya kutoa heshima kwa Bara la Afrika kwa kuwa Waafrika walioleta mafanikio hawaheshimiwi na kuenziwa ipasavyo humu humu Barani Afrika, na kwa sababu hiyo pengo hilo linazibwa kwa kupewa tuzo ya digrii za uzamivu za heshima. Walengwa hasa ni watu maarufu na viongozi ikiwa ni pamoja na Marais na Mawaziri wa nchi zetu za Kiafrika, Wabunge, n.k.

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inaamini kuwa huu ni upotoshaji na kukwepa ukweli kwamba kwa hakika digrii nyingi za aina hii zinatolewa kwa misingi ya kubadilishana fedha au kutangaza umaarufu wa taasisi husika. Mfano wa taasisi za aina hii uliandikwa katika makala iliyotolewa hivi karibuni katika gazeti la “The Guardian” la hapa nchini la Jumatatu tarehe 19 Julai, 2010 ikihusisha taasisi moja ya kidini nchini Marekani. Imethibitika kuwa anwani ya mahali ilipo taasisi hiyo haiko bayana na taasisi hiyo haitambuliwi na nchi yoyote ya Kiafrika na hata nchini Marekani kwenyewe.

Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania inapenda kutahadhalisha umma kuhusu kuwepo kwa matukio haya na kutoa ushauri kwa yeyote anayehusika kuwasiliana na Tume kwa ajili ya ushauri na uthibitisho wa masuala yote yanayohusu elimu ya juu ili kuepuka kutumia gharama kubwa zisizo za lazima kupitia njia za mkato na hatimaye kutunukiwa “digrii ya kutengenezwa”, digrii isiyokuwa na thamani, iwe ya heshima au vinginevyo.

Prof. Mayunga H.H. Nkunya
KATIBU MTENDAJI
TUME YA VYUO VIKUU TANZANIA